SOMO: KWANINI NI LAZIMA UWE TAJIRI
KWANINI NI LAZIMA UWE TAJIRI;1. Yesu ameivunja laana ya torati (kuanzia Kumbukumbu 28:15 na kuendelea, ambayo kati ya laana zilizoko hapo ni umasikini wa kipato na uchumi): Galatia 3:13-14.
2. Yesu amefanyika masikini ili wewe uwe tajiri kwa umasikini wake (2Kor 8:9).
3. Yesu alipofufuka na kushinda mauti, Mfumo wa utawala kwenye ulimwengu wa roho ulibadilika, toka kwa Shetani, na akawa kisheria na mamlaka yote na katika kila eneo (Mathayo 28:18).
4. Kilichomleta Yesu duniani ni “kutafuta na kuokoa kilichopotea” (Luka19:10, Mathayo 18:11), na kati ya vilivyokuwa vimepotea ni Uchumi wa mwanadamu uliokuwa mikononi mwa Shetani (Luka 4:5-7, Mathayo 4:8-9).
Na hiyo kazi pia aliimaliza na kuchukua mamlaka na nguvu ya Shetani kwenye eneo la uchumi (Yohana 17:4).
5. Yesu alipokuwa duniani alitembea kwenye “uchumi mkubwa” na hakuwahi kuwa masikini wa kukosa alichohitaji: Alilisha maelfu kwa chakula kidogo, alitatua matatizo ya kiuchumi kwa hekima ya Kiungu… Na Yesu huyuhuyu anakaa ndani yako na hajabadilika: NI YEYE YULE LEO KAMA ALIVYOKUWA JANA (Waebrania 13:8).
6. Yesu alifundisha kuhusu uchumi kupitia mfano wa “talanta” (Mathayo 25:14-29), na hapo alitufundisha tofauti ya KUWEKA AKIBA NA KUWEKEZA… Wale wawili WALIWEKEZA KILE WALICHOPEWA KAMA MTAJI na wakapata ASILIMIA MIA YA WALICHOWEKEZA (Mwenye tano alipata faida tano, mwenye mbili alipata faida ya mbili), Yule ALIYEIWEKA AKIBA ilibaki hivyohivyo na haikuongezeka. Baada ya muda alikuwa na KIASI KILEKILE ALICHOTUNZA kikiwa kimeshuka thamani kwakuwa fedha hushuka thamani kutegemea muda na dawa pekee ni KUIWEKEZA.
Yesu asingetufundisha siri hii kama anataka tuwe na uchumi mdogo!
7. Yesu hakushughulika na maswala na mahitaji ya kiroho na ya mwili tu ya waliomjia bali pia ALIFANYA MIUJIZA KWENYE ENEO LA UCHUMI PIA… Alifanya muujiza kwenye uchumi wa Petro (Luka 5), Kama uchumi si kipaumbele cha Yesu, asingefanya kitu hiki na miujiza mingi ya kiuchumi.
8. Nguvu ya kupata utajiri na uchumi mkubwa iko mikononi mwa Mungu (Kumbukumbu 8:18).
9. Kama unaamini kwenye BARAKA ZA MUNGU basi amini kwenye UTAJIRI PIA maana “Baraka ya Mungu hutajirisha” (Mithali 10:22).
Huwezi kubarikiwa na Mungu na usiwe na uchumi mkubwa na utajiri wa kutosha.
Ibrahim alipobarikiwa, uchumi wake uligeuka (Mwanzo sura ya 12 na 13:2).
Na Mungu huyu amekupa nafasi ya kuwa “mrithi wa ahadi na baraka za Ibrahimu” (Wagalatia 3:29, Wagalatia 4:28).
10. Mungu tunayemuabudu katika Kristo Yesu ndiye anayehusika na suala la KUTAJIRISHA WATU (Mhubiri 5:19, 1Samweli 2:7-8).
11. Bwana Yesu alisema atatuhukumu siku ya mwisho kwa kutegemea “tuliwavika, tuliwanywesha, tuliwalisha wahitaji na masikini” (Mathayo 25:31-46).
Na haya hayawezi kufanyika ukiwa masikini. Na Mungu hawezi kukupa kazi hii ya kulisha, kuvika, kunywesha, kusaidia wahitaji bila kukupa uchumi mkubwa wa kukurahisishia kazi hii ili akikuhukumu usije kujitetea kwamba ulikuwa masikini.
12. Kama una moyo wa kukubali “majukumu na uwajibikaji” ili kuleta nuru na majibu ya watu wengine, huwezi kuwa masikini (Isaya 60:1-4, 10-11, 16-22).
Ukiwa masikini umetaka, si Biblia wala Ufalme wa Mungu unaotaka uwe masikini.
Amka, lichukue Neno la Mungu na ulidai litimie maishani mwako.
NB: Fuatilia kila andiko na kuliweka katika maombi na matendo, kitaeleweka!
Mwl Dickson Cornel Kabigumila (Mwl D.C.K),
0753 466 675/ 0655 466 675